Timu ya Taifa (Taifa Stars) imeingia
kambini jana jioni (Desemba 12 mwaka huu) jijini Dar es Salaam kujiandaa
kwa mechi ya kirafiki ya kimataifa dhidi ya mabingwa wa Afrika, Zambia
(Chipolopolo) huku Kocha Kim Poulsen akimjumuisha tena katika kikosi
hicho kipa Deogratias Munishi ‘Dida’.
Kocha Poulsen amemjumuisha tena
Munishi kwenye kikosi hicho kuziba nafasi ya Mwadini Ally ambaye atakuwa
nje ya nchi na timu yake ya Azam inayokwenda kushiriki mashindano
maalumu nchini Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC).
Wachezaji wote wengine walioitwa
Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager wamesharipoti
kambini hoteli ya Tansoma, na timu imeanza mazoezi leo asubuhi (Desemba
13 mwaka huu) Uwanja wa Karume, na jioni itafanya mazoezi kwenye uwanja
huo huo.
Kuanzia kesho jioni (Desemba 14 mwaka
huu) itafanya mazoezi Uwanja wa Uwanja wa Taifa wakati mazoezi ya
asubuhi yataendelea kuwa Uwanja wa Karume. Wachezaji ambao bado
hawajaripoti kambini ni Mbwana Samata na Thomas Ulimwengu wanaocheza
mpira wa kulipwa nchini DRC.
Mechi kati ya Taifa Stars na mabingwa
hao wa Afrika itachezwa Desemba 22 mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa.
Kocha wa Chipolopolo, Herve Renard ameshataja kikosi chake cha wachezaji
24 kwa ajili ya mechi hiyo.
COASTAL YAENDELEA KUCHACHAFYA UHAI CUP 2012
Coastal Union ya Tanga imeendelea
kufanya vizuri kwenye michuano ya kuwania Kombe la Uhai inayoshirikisha
wachezaji wenye umri chini ya miaka 20 wa klabu za Ligi Kuu ya Vodacom
baada ya jana (Desemba 12 mwaka huu) kuifunga Toto Africans mabao 3-1.
Mabao ya Coastal katika mechi hiyo ya
kundi A iliyochezwa Uwanja wa Chamazi yalifungwa na Mohamed Miraji
dakika ya 44, Abdul Banda (dk. ya 62) na Ramadhan Shame (dk. ya 83).
Toto Africans ndiyo iliyoanza kupata bao dakika ya 30 lililofungwa na
Severin Constantine.
Coastal Union ilishinda mechi yake ya
kwanza mabao 2-1 dhidi ya Tanzania Prisons katika michuano hiyo
inayodhaminiwa na kampuni ya Said Salim Bakhresa kupitia maji Uhai.
Nayo Simba iliibuka na ushindi wa
mabao 2-1 dhidi ya African Lyon katika mechi ya kundi B iliyochezwa leo
asubuhi (Desemba 12 mwaka huu) Uwanja wa Karume. Miraji Athuman na
Ramadhan Mzee ndiyo walioifungia Simba dakika ya 15 na 47 wakati la
African Lyon lilifungwa dakika ya 57 na Mbela Kashakala.
Polisi Morogoro iliifunga Azam bao
1-0 kwenye Uwanja wa Karume wakati katika Uwanja wa Azam, JKT Ruvu
iliifunga Tanzania Prisons bao 1-0 lililofungwa dakika ya 16 na Jacob
Mambia. Yanga na Ruvu Shooting zilitoka suluhu kwenye Uwanja wa Chamazi.
Katika mechi iliyochezwa leo asubuhi
(Desemba 13 mwaka huu) Uwanja wa Karume, Oljoro JKT imeizamisha Kagera
Sugar mabao 3-0. Mabao hayo yamefungwa na Hamis Saleh dakika ya 49 huku
Shamir Mohamed akipachika mawili dakika ya 52 na 55.
Michuano hiyo itaendelea kesho
(Desemba 14 mwaka huu) kwa michezo kati ya Mtibwa Sugar vs Toto Africans
(asubuhi- Karume), Coastal Union vs JKT Ruvu (mchana- Karume), Oljoro
JKT vs Yanga (asubuhi- Chamazi), Ruvu Shooting vs Kagera Sugar (mchana-
Chamazi), Mgambo Shooting vs Simba (asubuhi- Chamazi) na African Lyon vs
Azam (jioni- Chamazi).
0 comments:
Post a Comment