Sherehe za siku ya wafanyakazi duniani zilizoadhimishwa kote ulimwenguni hapo jana, zilitawaliwa na mgomo nchini Tanzania huku Rais Jakaya Kikwete akiahidi nyongeza ya mishahara. Madereva wa mabasi yanayofanya safari kwenda mikoani na nchi za jirani, jana walifanya mgomo katika Kituo Kikuu cha Mabasi, Ubungo, Dar es Salaam wakishinikiza mikataba yao ya ajira. Mgomo huo uliodumu kwa takribani masaa sita, mbali na suala hilo la mikataba, madereva hao pia waligoma wakitaka waajiri wao kuwalipa mishahara isiyopungua kima cha Sh 350,000 kwa mwezi na posho za safari, kutokana na kazi wanayoifanya. Mgomo huo ulikwamisha safari za kwenda mikoani na kuleta usumbufu mkubwa kwa wasafiri waliokuwa wakisubiri kusafiri kuelekea mikoani na nchi jirani za Kenya na Uganda. Wakati huo huo, Rais Jakaya Kikwete wa Tanzania aliwahutubia maelfu ya wafanyakazi na Watanzania kwa ujumla katika sherehe za Siku ya Wafanyakazi Duniani zilizofanyika kitaifa kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro na kuwahakikishia wafanyakazi kote nchini humo kwamba, serikali yake itaendelea kuboresha maslahi yao kila mara uwezo unaporuhusu.
0 comments:
Post a Comment