Mamilioni ya Mashia duniani waomboleza kumbukumbu ya Ashura
Mamilioni ya Waislamu wa madhehebu ya Shia kote duniani hii leo wameshiriki katika maombolezo ya kumbukumbu ya Ashura yaani siku aliyouawa shahidi mjukuu wa Mtume Muhammad SAW, Imam Hussein AS. Imam Hussein AS pamoja na masahaba wake watiifu wapatao 72 na familia yake waliuawa shahidi kikatili katika jangwa la Karbala, Iraq katika vita baina ya haki na batili vilivyotokea mwaka 61 Hijria. Katika vita hivyo jeshi la batili lilikuwa likiongozwa na Yazid bin Muawiya huku jeshi la haki likiongozwa na Imam Hussein bin Ali AS mjukuu wa Bwana Mtume SAW. Nchini Iran misikiti, Husseiniya, viwanja na barabara za miji yote leo zilifurika waombolezaji wa maombolezo hayo ambayo yanakumbusha jinsi Imam Hussein AS na masahaba zake walivyoamua kutoa roho zao kwa ajili ya kulinda Uislamu. Maombolezo ya siku aliyouawa shahidi Imam Hussein AS ambayo ni maarufu kama siku ya Ashura ni nembo ya msimamo wa haki dhidi ya batili na mapambano ya mwanadamu dhidi ya dhulma na madhalimu.
0 comments:
Post a Comment