Ujerumani imeiadhibu Argentina kwa kuifunga mabao 4-0 kwenye mechi ya robo fainali ya Kombe la Dunia katika uwanja wa Green Point mjini Cape Town na kujipatia nafasi katika nusu fainali.
Juhudi za Ujerumani kutaka kufuzu miongoni mwa nne bora zilianza katika dakika ya tatu wakati Thomas Muller alipofunga kwa kichwa mpira wa adhabu uliopigwa na Bastian Schweinsteiger.
Kipindi cha kwanza kilimalizika Ujerumani wakiongoza 1-0 na katika dakika ya 68, Miroslav Klose akiichezea nchi yake mechi ya 100 aliongeza bao la pili kukamilisha pasi ya Lukas Podolski.
Podolski aliendelea kupenyeza pasi za kupendeza kutokea upande wa kushoto, na katika dakika ya 74 alitoa moja ambayo mlinzi Arne Friedrich alifunga bila matatizo, na kuipatia Ujerumani bao la 3.
Klose alipata fursa nyingine katika dakika ya 89 kumalizia pasi nyingine kutoka Podolski na kuandikisha bao lake la pili, na la nne kwa Ujerumani.
0 comments:
Post a Comment