Mke wa Rais Mama Salma Kikwete (kulia) katika mkutano wa African First Ladies Roundtable jijini New York, Marekani.
Na Anna Nkinda – Maelezo, New York
Mshikamano
wa pamoja unahitajika baina ya nchi zilizoendelea na zinazoendelea ili
kuhakikisha kuwa mtoto wa kike ambaye hajapata nafasi ya kwenda shule
anapata elimu, kuwainua wanawake kiuchumi na kupunguza vifo vya kinamama
wajawazito na watoto vinavyotokana na tatizo la uzazi na ugonjwa wa
kansa.
Hayo
yamesemwa jana na Mke wa rais Mama Salma Kikwete wakati akichangia
mada kwenye mkutano wa Wake wa Marais uliofanyika makao Makuu ya
Taasisi ya Ford mjini New York nchini Marekani.
Mama
Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa Taasisi ya Wanawake na Maendeleo
(WAMA) alisema kuwa taasisi mbalimbali za Kiserikali na zisizo za
kiserikali zinafanya jitihada kubwa ya kuhakikisha kuwa zinawasaidia
wanawake wanaokabiliwa na changamoto mbalimbali za maisha tatizo
lililopo ni upungufu wa rasilimai fedha za kuweza kukabiliana na
changamoto hizo hivyo basi ushirikiano wa pamoja unahitajika ili kuweza
kufanikisha malengo hayo.
Aliendelea
kusema kuwa watoto wa kike wakipata elimu ya kutosha watakuwa na silaha
muhimu katika maisha yao ya kuweza kupambana na matatizo mbalimbali
ikiwa ni pamoja na maradhi, ujinga na umaskini kwani elimu ni nguzo
muhimu katika maendeleo ya taifa lolote Duniani bila ya watu kuwa na na
elimu nchi haiwezi kuendelea.
“Ukimuelimisha
mtoto hasa mtoto wa kike ambaye amekosa nafasi ya kupata elimu ni
faida kwa mtoto, Taifa na Dunia kwa ujumla kwani hivi sasa tumejionea
wanawake wengi wakishika nafasi za juu za uongozi kitaifa na Dunia pia
wameweza kujikwamua kiuchumi tofauti na miaka ya nyuma”, alisema Mama
Kikwete.
Mwenyekiti
huyo wa Taasisi ya WAMA alisema kuwa nchini Tanzania watoto wengi
wa kike ambao ni yatima na wanaishi katika mazingira hatarishi
wameshindwa kupata elimu sawa na watoto wengine hivyo basi aliamua
kuanzisha taasisi hiyo ili aweze kuwasaidia watoto hao, kuwainua
wanawake kiuchumi na kupunguza vifo vya kina mama wajawazito na watoto
na wanaougua ugonjwa wa kansa kwa kutoa elimu kwa wananchi na vifaa
tiba katika vituo vya afya na Hospitali .
Mkutano
huo wa siku moja ulihudhuriwa na wake wa marais na wakuu wa Serikali wa
Afrika, mke wa rais mstaafu wa Marekani Laura Bush na mke wa waziri
Mkuu Mstaafu wa Uingereza Cherie Blair, pamoja na viongozi mbalimbali wa
Serikali na mashirika binafsi kutoka nchi wa Afrika na Marekani.
Katika
mkutano huo mambo mbalimbali yalijadiliwa ikiwa ni pamoja na
kuangalia jinsi gani wake wa maraisi na wakuu wa Serikali wanaweza
kuleta mabadiliko katika nchi zao katika kuimarisha afya ya mwanamke,
kuhakikisha kuwa mtoto wa kike anapata elimu na na kuwainua wanawake
kiuchumi pamoja na changamoto wanazoweza kukabiliana nazo.
0 comments:
Post a Comment