Inter Milan ya Italia imethibitisha kuwa imemfukuza kazi meneja Rafael Benitez, miezi sita tu baada ya kuteuliwa kuiongoza klabu hiyo.
Hatua hiyo imekuja baada ya Benitez kutaka kuungwa mkono ndani ya bodi ya wakurugenzi kununua wachezaji, kufuatia klabu hiyo kushinda kombe la dunia la vilabu, kwa kuifunga TP Mazembe siku ya Jumamosi.
Badala yake, Inter, ambayo inasuasua katika nafasi ya saba kwenye msimamo wa ligi ya Serie A, imeamua kumfukuza kazi Benitez.
Mourinho, ambaye aliondoka Inter na kwenda Real Madrid ya Uhispania, aliiongoza timu hiyo kuchukua ubingwa wa ligi ya Italia na klabu bingwa Ulaya msimu uliopita na kumuachia Benitez kazi ngumu ya kufuata nyayo zake.
Ingawa Inter ina kiporo cha mechi mbili dhidi ya timu zilizo juu yake, imeshinda mechi sita tu kati ya mechi 15 za ligi.
katika kutetea ubingwa wao wa klabu bingwa, Inter imeweza kumaliza katika nafasi ya pili ya makundi, nyuma ya Tottenham ya England, na kuiacha katika wakati mgumu kwani itapambana na Bayern Munich katika raundi ya timu 16.
"Kuna njia tatu hapa," alisema Benitez. "Moja, kuungwa mkono kwa asilimia 100 kwa meneja na kununua wachezaji wanne au watano kuunda kikosi imara na kuendelea kushinda mataji na mechi.
"Mbili, kuendelea hivi hivi bila ya mpango wala mwelekeo na kuendelea kumlaumu mtu mmoja msimu mzima.
"Na tatu" aliongeza Benitez, "ni kuzungumza na mwakilishi wangu na kufikia makubaliano iwapo hakuna kuungwa mkono. Rahisi kabisa."
Rais wa Inter Massimo Moratti hakupendezwa na matamshi hayo ya Benitez na kusema "hayakuwa sahihi kwa hali ilivyo" kabla ya kuongeza kusema huu si "wakati wa kuomba kuimarisha kikosi".
0 comments:
Post a Comment