Sudan yajieungua kushiriki katika mkutano wa viongozi wa Afrika na Ulaya
Serikali ya Sudan imesema kuwa, haitoshiriki katika kikao cha viongozi wa Umoja wa Afrika na Umoja wa Ulaya ambacho kinaanza leo katika mji mkuu wa Libya, Tripoli. Serikali ya Sudan imesema kwamba, mbali na Rais Omar al-Bashir kutoshiriki katika kikao hicho hakuna kiongozi au mwakilishi yeyote wa Sudan ambaye atashiriki katika kikao hicho. Serikali ya Khartoum imesema kuwa, imeamua kususia mkutano huo kutokana na mashinikizo ya madola ya Ulaya dhidi ya nchi za Kiafrika na kama Rais al-Bashir atashiriki mkutano huo. Taarifa ya serikali ya Khartoum imebainisha kwamba, mashinikizo na msimamo wa madola ya Ulaya kuhusiana na ushiriki wa Rais wa Sudan katika kikao cha Libya inabainisha fikra za kikoloni walizonazo viongozi wa Ulaya kwa bara la Afrika. Rais wa Sudan anatakiwa na Mahakama ya Kimataifa ya Jinai ICC ambayo kwa nyakati tofauti imetoa waranti mbili hadi sasa zinazotaka kutiwa mbaroni Rais Bashir kwa tuhuma za kuhusika na jinai za kivita. Waranti ya kwanza ilitolewa mwaka uliopita ambapo ICC inadai kwamba rais wa Sudan ametenda jinai za kivita katika eneo la Darfur. Mwezi Julai mwaka huu ICC ikatoa waranti ya pili baada ya kuongeza tuhuma za mauaji ya kimbari katika faili la Al-Bashir.
0 comments:
Post a Comment