Maimamu wa Jamaa nchini Uhispania walalamikia marufuku ya Hijab
Maimamu wa sala ya Jamaa katika Misikiti kumi na moja iliyoko katika jimbo la Catalonia nchini Uhispania wamechukua uamuzi wa kufungua mashtaka mahakamani wakilalamikia njama za viongozi wa eneo hilo la kupiga marufuku uvaaji wa hijabu yaani vazi la stara la mwanamke wa Kiislamu. Sheikh Farid Khutuut Msaidizi wa Mkuu wa Taasisi ya Kiutamaduni ya Kiislamu na Mjumbe wa Baraza la Utendaji katika jimbo la Catalonia amesema kuwa, taasisi hiyo ina azma kufungua mashtaka dhidi ya njama hizo zilizo kinyume cha sheria. Naye Elisa Sanchez Camacho Mbunge wa Baraza la Seneti la Uhispania ameunga mkono mpango wa kupigwa marufuku uvaaji wa hijabu nchini humo na kudai kuwa, wananchi wa Uhispania wanaamini kwamba utumiaji wa burqa na niqabu unakiuka utukufu na heshima ya mwanamke. Duru zinazofungamana na Chama cha Kitaifa cha Uhispania zinasema kuwa, uamuzi wa kupiga marufuku uvaaji wa niqabu na burqa ni juhudi za kukabiliana na mwenendo unaozidi kuongezeka za kuwashawishi wanawake wa Kihispania kuvaa mavazi hayo na kusisitiza kuwa, iwapo uamuzi huo utapitishwa unaweza kuleta athari na mlingano wa pamoja na nchi nyingine za Ulaya za kupiga marufuku uvaaji wa niqabu na burqa barani humo.
0 comments:
Post a Comment