Searching...
Friday, July 20, 2012

HOTUBA YA RAIS WA ZANZIBAR KWA MWEZI MTUKUFU WA RAMADHAN LEO

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk. Ali Mohamed Shein amewataka wafanyabiashara kufanya biashara zao kwa misingi ya kutodhulumiana katika bei, viwango na vipimo hasa katika mwezi mtukufu wa Ramadhani.

Dk. Shein aliyasema hayo leo wakati alipokuwa akisoma risala ya Ramadhani  kwa wananchi kupitia vyombo vya habari kwa mwaka huu wa 1433 Hijriya sawa na mwaka 2012 Miladia.


Katika maelezo yake Alhaj Dk. Shein alisema kuwa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani ni wa neema kibiashara lakini ni vyema kufanya neema hiyo iwe kwa wauzaji na kwa wanunuzi.


Alieleza kuwa Muuzaji anauza bidhaa zake nyingi  zaidi kwa hivyo anapaswa kuhakikisha zina ubora na anachuma faida kwa kiasi ya anachouza.


Aidha, alisema kuwa mnunuzi naye anahitaji kupewa bei iliyo nafuu hasa kwa bidhaa ambayo Serikali imeipunguza kodi, kwani Serikali kama kawaida itapunguza ushuru kwa biadhaa muhimu za chakula ili

kuwawezesha wananchi kupata unafuu wa bei.

“Ni jambo la kusikitisha kuona baadhi ya wafanyabiashara wenye tamaa wanasafirisha bidhaa kama vile unga, sukari na mchele walizotozwa kodi ya chini na kuzisafirisha kwa njia ya magendo nje ya Zanzibar ili wapate faida kubwa’,alisema Alhaj Dk. Shein.

Kutokana na mambo hayo Alhaj Dk. Shein alisema kuwa husababisha upungufu wa baadhi ya vyakula na kuwasababishia shida wananchi wakati huu  wa mwezi wa Ramadhani.


Pamoja na hayo, Alhaj Dk. Shein alitoa shukurani kwa wakulima nchini kwa kujiandaa kuwaopa huduma nzuri wananchi hasa katika upatikanaji wa chakula kwa ajili  ya futari huku akieleza kuwa serikali imeweka

mazingira mazuri ya biashara hasa katika Mwezi huo wa Ramadhani.

Alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar nayo itajitahidi kufanya kila linalowezekana ili kuwasaidia wananchi katika kukabiliana na tatizo la upatikanaji wa maji katika maeneo mbali mbali nchini.


Alhaj Dk. Shein alisema kuwa Serikali imo katika juhudi za kuwaandalia wananchi wake maisha bora, kwa kupitia mageuzi ya katiba na pia kwa kuhesabiwa watu, mambo ambayo yamo katika sheria.

0 comments:

WELCOME URARY95 SPORTS NEWS BLOG | ADVERTISE YOUR BUSINESS HERE AT A CHEAP PRICE MORE INFORMATION CONTACT US: 0654315901 | Email: urary95@yahoo.com | KARIBU URARY95 SPORTS NEWS BLOG | TANGAZA BIASHARA YAKO HAPA KWA GHARAMA NAFUU KWA MAELEZO ZAIDI WASILIANA NASI: 0654315901 | Barua Pepe: urary95@yahoo.com
 
Back to top!